Mzee wa tafakari

Tuesday, January 23, 2007

HakiElimu imeadhibiwa kwa kusema ukweli


WIKI hii serikali lifanya maamuzi mazito ya kulipiga marufuku shirika lisilo la kiserikali la HakiElimu kuchapisha taarifa au ripoti zinazohusiana na shule za Tanzania.

Uamuzi wa serikali upo katika waraka wake ambao unalipiga shirika hilo kufanya utafiti na kutoa vitabu na machapisho yoyote katika shule za awali, msingi, sekondari na vyuo vya ualimu.

Sababu ambayo serikali imetoa kwa kulipiga marufuku shirika hilo ni kuwa limekuwa likitoa matangazo ya kudhalilisha serikali kwa kubeza mafanikio ya elimu yaliyopatikana na kwamba hatua hiyo inatoa picha mbaya kwa wananchi.

Moja ya matangazo hayo yanaonekana yanaiudhi ni lile linalotolewa katika redio na televisheni likieleza jinsi baadhi ya wakuu wa shule wanavyotumia vibaya fedha za Mpango wa Elimu kwa Shule za Msingi nchini (MMEM).

Sababu nyingine ambayo imetajwa na serikali ni kushindwa HakiElimu kufuata mwongozo iliyopewa na wizara ya Elimu na Utamaduni licha ya kuonywa mara kwa mara.

Kwa hakika, uamuzi huu unasikitisha kwa sababu hakuna mpenda maendeleo yoyote ambaye anaweza kuchekelea uamuzi huu hata kidogo.

Nasema kwa mpenda maendeleo hauwezi kumfurahisha kwa sababu ni dhahiri unaziba mwanya wa upashanaji habari na uimarishaji wa mijadala ya kidemokrasia.

Hivi kweli yanayosemwa katika matangazo ya Hakielimu hayapo hapa nchini? Ni swali ambalo tunajiuliza.

Tunajua kuwa kuna maendeleo makubwa yaliyofikiwa katika sekta ya elimu nchini na serikali ya awamu ya tatu, lakini pia lazima tukiri pia kuna upungufu upo ambao unaweza kuwa kikwazo cha kufikia mafanikio makubwa zaidi. Upungufu huu unaweza kuwa unachangiwa baadhi ya watendaji katika Wizara ya Elimu na Utamaduni.

Wizara ya Elimu na Utamaduni ambayo inajukumu la kusimamia elimu nchini, ina wajibu pia wa kuangalia na kufuatilia yanayosemwa na vyombo vingine badala ya kuchukua uamuzi wa kuvifunga mdomo.

Dalili za kutaka kuifunga HakiElimu mdomo zilianza kujionyesha siku nyingi baada ya Waizri wa wizara hiyo, Joseph Mungai kulalamika kuwa matangazo yanayotolewa na shirika hilo yanamwudhi kwa vile yanabeza mafanikio yaliyopatikana.

Mimi naamini kuwa uamuzi wa kuifunga mdomo Hakielimu ambao manadalizi yake yalianza siku nyingi, umechukuliwa kwa sababu nyingine na sio hizo za zinazotajwa katika waraka.

Nasema sio hizo kwa sababu, kama suala la baadhi ya wakuu wa shule kutumia fedha za elimu bila ya kufuata utaratibu lipo na baadhi yake wamefunguliwa mashtaka, kwa nini serikali leo iseme ni uongo!

Tatizo la baadhi ya walimu kushindwa kufuata taratibu za ufundishaji bora nalo lipo na limekuwa likizungumza mara kwa mara hata na Mungai mwenyewe, sasa kitu gani kilichopikwa na HakiElimu?

Hakuna shaka kwamba HakiElimu ni mdau wa elimu Tanzania inaweza kuchagia mawazo, kushiriki katika kutoa michango, kuamsha mawazo mapya na kutoa changamoto zinazokwenda na mahitaji ya kizazi cha sasa katika nchi hii.

Tunashawishika kama nilivyosema hapo awali kuwa uamuzi huu umechukuliwa na serikali huenda kwa ajili ya joto la uchaguzi na sio kwa sababu kuwa kinachosema na HakiElimu hakipo.

Hata hivyo, Mungai anapaswa kuelewa kuwa matangazo ya HakiElimu hayawezi kuwashawishi wapigakura kubadilisha mawazo yao kutompigia kura chama au mgombea wanayemtaka.

Hatua ya kupiga ya serikali marufuku HakiElimu ni jambo ambalo limezua mjadala mzito kuwa huenda sasa serikali imeamua kufunga uhuru wa mashirika yasiyo ya kiserikali ambayo yanaonekana kupata umaarufu kama ilivyowahi kufanya kwa Barala la Wananke Tanzania (BAWATA).

Kwa nchi inayofuata utawala wa sheria, inayoheshimu mgawanyo wa madaraka na dhana nzima ya kudhibitiana katika utendaji, ni jambo lisilokubalika kwa Wizara ya Elimu na Utamaduni kuwa mlalamikaji, mwendesha mashitaka, hakimu na wakati huo huo kuwa magereza.

Utaratibu wa namna hiyo hauruhusu haki kutendeka hata kidogo.

Ni vizuri serikali na vyombo vyake vyote vikafahamu kwamba hizi ni enzi za uwazi katika kushirikishwa wadau katika mambo yote yanaowahusu maendeleo ya wananchi.

Serikali kuendesha kila kitu itakavyo bila kutafuta na kuzingatia maoni ya wale walioko nje ya mfumo wa serikali ni kufuata utawala usio wa sheria.

Kama nilivyosema awali HakiElimu wamekuwa wakitoa maoni yao kuhusu yale yanayotendeka katika mashule wala hawako kwa ajili kuipaka matope serikali.

Mungai anataka kuwalazimisha watanzania kuimba wimbo wa kusifia tu mafanikio yaliyopatikana wakati tunaona yamezingirwa na baadhi ya matatizo ambayo yakiondoka, maendeleo hayo yanaweza kuonekana kwa urahisi na watu wengi.

Kinachoonekana hapa ni kuwa HakiElimu ni mtoto ambaye ameadhibitiwa sababu tu kamwona baba yake yuko uchi na akamwambia baba uko uchi jifunike.

Ina maana gani kama utamwacha baba akiwa uchi usimwambie halafu watu wote mtaa mzima wakamwona!

Jamani hata ng'ombe anayesubiri kuchinjwa hutunzwa!

WIKI hii Mwenyekiti wa Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora, Jaji Robert Kisanga, alitoboa siri iliyojificha kwa muda mrefu nchini kuhusu maisha ya wafungwa na mahabusu katika magereza.

Alisema tume yake imebainisha kuwapo kwa ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu katika magereza nchini ambako wafungwa na mahabusu watoto wanawekwa pamoja na watu wazima hali inayosababisha kulawitiwa.

Hata hivyo, Jaji Kisanga alisema tume hiyo ilisema kuwa kumekuwa na usiri mkubwa katika suala zima la ulawiti baina ya wafungwa na maafisa wa Magereza.

Alisema kutotengwa sehemu kwa watoto wadogo na watu wazima, limeelezwa kuwa ndicho chanzo cha ulawiti magarezani na hivyo kuathiri juhudi za mapambano dhidi ya ukimwi magerezani na kwamba kumejitokeza usiri juu ya suala la kulawiti katika pande zote maafisa wa Magereza, wafungwa na mahabusu wenyewe.

Maelezo ya Jaji Kisanga ni matokeo ya ziara ya Tume ya kukagua Magereza na kambi za Magereza 15 na vituo vya polisi 42 katika wilaya 20 za Tanzania Bara kwa mwaka 2004/2005.

Miongoni mwa Magereza na kambi zilizokaguliwa ni pamoja na Kongwa, Mpwapwa mkoani Dodoma, Muleba (Kagera), Kilosa (Morogoro), Magu, Butimba (Mwanza), Kahama na Shinyanga.

Katika magereza 15 yaliyokaguliwa na Tume ni gereza la Kongwa (Dodoma) tu ambalo lina bweni la watoto, yaliyobaki watoto waliwekwa katika chumba kimoja na watu wazima, hali hiyo ni ukiukwaji wa haki za watoto na pia inahatarisha maisha ya watoto kisaikolojia.

Pia magereza hayo yaliyotembelewa na kukaguliwa zaidi ya asilimia 50 yalikuwa na msongamano mkubwa wa wafungwa na mahabusu na kwamba hali hiyo inahatarisha maisha na ni uvunjwaji wa haki za binadamu na misingi ya utawala bora.

Kwa hakika ripoti hiyo inatufumbua macho kujua hali ya magereza yetu yalivyogeuka kuwa jehanamu badala ya kuwa eneo la kurekebisha tabia za wafungwa.

Hivi sasa mtu akipatikana na kosa hata la kuiba chungwa akifungwa jela miezi sita ni sawa na amefungwa kifungo cha maisha kwa vile huwa hana uhakika kama anatarejea salama au atakufa kutokana na mazingira mabaya yaliyopo katika magereza.

Vitendo na mazingira yaliyoelezwa na tume ya Jaji Kisanga kwamba mahabusu watoto na wafungwa wakubwa kuwekwa katika chumba kimoja kwa hakika ni ni cha hatari na kinahatarisha maisha ya watoto hao.

Nashindwa kuelewa uamuzi huo wa kuwachanganya mahabusu watoto na wafungwa wakubwa unafanywa kutokana na na nini? Ni uhaba wa vyumba vya magereza kutunzia wafungwa au kitu gani? Nadhani waziri wa Mambo Ndani ya Nchi, John Chiligati anapaswa kutueleza watanzania.

Mbali ya kulawitiwa watoto katika magereza lakini hata hali ya magereza bado haziridhishi. Magereza mengi vyumba vya mahabusu vingi vina mwanga mdogo kutokana na kuwa na madirisha madogo au kutokuwa na madirisha kabisaa.

Pia vyumba hivyo mbali ya kutokuwa na mwanga lakini ni vidogo ambavyo wafungwa wanalala wengi wakiwa wamekaa kutokana na kukosa nafasi pamoja na kujisaidia katika ndoo jambo ambalo limekuwa likisababishia wafungwa hao kupata magonjwa wa milipuko kama kipindupindu na kuhara damu.

Hivi kweli hata kama wafungwa ni wahalifu ni haki kuwaweka katika chumba ambacho hakina mwanga na kidogo ambacho hawezi hata kulala. Kwa maana nyingine ni kwamba mtu akikaa mahabusu kwa miaka mitatu atakuwa hawezi kupata sehemu ya kulaza ubavu wake katika kipindi chote hicho? Hii ni njia bora ya kuwarekebisha tabia wafungwa kweli ili wakitoka wawe raia wema au ni njia ya kuwaua?

Kwa maana nyingine ni kwamba wafungwa na mahabusu wa Tanzania wanatumikia adhabu mara mbili ya kwanza ya kutokana na makosa waliyoyafanya na mazigira mabaya yaliyopo katika vyumba vya magereza.

Hata hadithi ya maarufu ya safari za Sindbad alipofika katika kisiwa cha wala watu walipokelewa kwa heshima na wenzake wakalishwa mapande ya nyama makubwa ili wanenepe kabla ya kuliwa.

Bahati yake Sindbad alikataa kuyala akakonda na kuonekana hafai kuwa chakula wa mfalme wa eneo hilo. Kwa maana nyingine hata kama waandhibiwa lakini utu wao kama binadamu unabaki pale pale.

Nadhani kufikiria kuwa kuweka mazingira ya magereza katika hali nzuri ni kuwafanya watu waendelee kufanya uhalifu ni makosa kwa vile kunyimwa uhuru aliokuwa nao wa kuwa uraiani, kuwa mbali na familia yake, ndugu zake, marafiki na kufanya kazi akiwa chini ya ulinzi mkali wa askari magereza ni adhabu tosha inayomfanya mtu akitoka kule amerekebishwa tabia yake.

Badala ya magereza nchini kuwa chuo cha mafunzo ya kurekebisha tabia hivi sasa yamekuwa ni kituo cha kupika wahalifu na wengi kufa wakiwa wanatumikia vifungo vya kutokana na kuugua ugonjwa mbalimbali yakwamo ya kifua, kikuu, ukimwi na kipindupindu.

Nadhani sasa umefika wakati kwa serikali iboreshe hali ya magereza yetu ili kweli yawe ni vyuo vya mafunzo ya kurekebisha tabia badala ya watu wanaotoka magerezani wanaingia mitaani wakiwa wamejifunza mbinu za uhalifu badala ya tabia nzuri.

Wafungwa wanaomaliza vifungu vyoa hasa vijana wamekuwa wakitoka magereza wakiwa wameharibikiwa zaidi kuliko hapo awali wengi wakiwa ni wavuta bangi hali ambayo inawafanya kujiingiza katika uhalifu na kurejea tena kutumikia vifungo.