Mzee wa tafakari

Tuesday, February 06, 2007

Sarungi hapo umepotoka

Profesa Philemon Sarungi amejizolea sifa na heshima nyingi kwa Watanzania kutokana na rekodi yake ya utumishi katika nyadhifa mbalimbali hapa nchini.

Sarungi ambaye ni Daktari bingwa wa mifupa anakumbukwa sana na Watanzania kutokana na mara kwa mara kurejea chumba cha upasuaji hospitalini kuhudumia wagonjwa kila bila ya kujali nyadhifa alizo nazo za ubunge na uwaziri.

Katika majanga makubwa ya kitaifa mchango wake mkubwa huonekana zaidi. Wakati huo huvaa nguo rasmi za utatibu na kuwashiriki bega kwa bega na madaktari wengine kuokoa maisha ya majeruhi.

Kwa hakika Profesa Sarungi ameonyesha jinsi ambavyo Watanzania wanatakiwa kuzitumia taaluma zao vyema katika kuwasaidia wenzao bila ya kuangalia kwamba hivi sasa wanafanya kazi zipi.

Hata hivyo, hivi karibuni utumishi mzuri wa Waziri huyu msomi aliyebobea ameanza kuupaka matope baada ya kutoa kauli bungeni ambayo inaonyesha dhahiri kuwa sasa anataka kutugoganisha raia askari wetu.

Kauli ya Waziri Sarungi ambayo nitazungumzia katika safu hii leo ni ile ambayo kuwaonya raia kuacha kuwachokoza askari wa majeshi yetu kwa namna yoyote ikiwamo kuwachukulia wake zao.

Sarungi alikaririwa akiwaasa wananchi kuwa wakiwachokoza kwa kuwatolea maneno yasiyofaa au kuwachukuliwa wakeza zao, wajue kuwa ugomvi wa askari mmoja huwa askari wote.

Kitu cha kushangaza katika kauli yake Sarungi alisahau kutuleza iwapo askari atamchukua mke wa raia yeye atafanywe nini?

Sarungi tunamheshimu Watanzania kama nilivyoeleza hapo awali, lakini kitendo cha kutoa kauli kama hiyo kinatushangaza.

Tunakubali kuwa raia hawapaswi kuwachokoza askari wetu kwa namna yoyote kwa sababu kwa kufanya hivyo ni kuvunja sheria za nchi, lakini kwa sababu nchi hii inaendeshwa kwa sheria na utawala bora pia hatutarajii askari kutoka jeshi lolote nchini akavamia raia na kufanya uchokozi.

Kwasababu tuna matukio kadhaa ambayo yametokea hapa nchini ya askari kuanzisha ugomvi dhidi ya raia na kwamba baada ya uchunguzi baadhi yao wengine wamefukuzwa kazi.

Kinachotisha ni kuwa kauli ya Sarungi hakugusia kuwaonya askari kama vile raia ni halali kuwafanyiwa vurugu.

Kwa vile, Watanzania sio utamaduni wetu wa kuwa na vurugu, tunaishi kwa kupendana na kuheshimiana, basi sheria ifuatwe kwa pande zote kama raia atamchokoza askari achukuliwe hatua za kisheria na hivyo hivyo kwa askari akimchokoza askari achukuliwe hatua za kisheria.

Kutoa kauli ya upande mmoja inaweza kuhamasisha baadhi ya askari kuhisi kuwa sasa wameruhusiwa kujichukulia sheria mkononi kuwaadhibu raia.

Kwa nchi ya amani inayofuata utawala wa sheria kama Tanzania hatuamini kama tumefikia mahali ambako tunashindwa kuishi na askari wetu kwa amani hadi kufikia mahali waziri kutoa kauli kama hiyo.

Moja ya majeshi ambayo yanasifika kwa askari wake kuwa na nidhamu duniani basi ni majeshi yetu ya Tanzania. Kutokana na kuwa na sifa hiyo ninaamini kuwa ni baadhi ya askari wachache ambao wamekuwa wakijiingiza katika ugomvi na raia.

Tunaamini ili kuondoa tatizo hili, basi sheria ichukue mkondo wake bila ya kubagua huyu ni nani na yule ni nani.

0 Comments:

Post a Comment

<< Home